Bodi ya Maziwa Tanzania
Wizara ya Mifugo na Uvuvi

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,

TDB Logo
TANZANIA, RWANDA KUSHIRIKIANA KUKUZA TASNIA YA MAZIWA
13 Jan, 2024
TANZANIA, RWANDA KUSHIRIKIANA KUKUZA TASNIA YA MAZIWA

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega na Waziri wa Kilimo, Maliasili, na Mifugo wa Jamhuri ya Rwanda, Mhe. James Kabarebe wamesaini hati ya makubaliano ya kushirikiana kuendeleza tasnia ya maziwa baina ya nchi hizo mbili.

Tukio hilo la utiaji saini limefanyika Visiwani Zanzibar  Januari 12, 2024 sambamba na Sherehe za Kutimiza Miaka 60 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.

Akizungumza katika tukio hilo, Waziri Ulega alisema kuwa ushirikiano huo ambao umekusudia kuendeleza viwanda vya usindikaji wa maziwa utasaidia kuongeza uzalishaji wa maziwa wa nchi hizo mbili jambo ambalo litapelekea kupatikana kwa ajira, usalama wa chakula na kukuza uchumi wa kaya na mtu mmoja mmoja kupitia mnyororo wa thamani wa maziwa.

Alisema kuwa mpaka sasa bado nchi inaagiza maziwa mengi kutoka nje ya nchi, lakini kupitia ushirikiano huo ana uhakika uzalishaji wa maziwa nchini utaongezeka na kuchechemua biashara baina ya nchi hizo mbili.

“Tanzania na Rwanda tumeamua kushirikiana katika mambo mbalimbali ya Maendeleo ya Tasnia ya Maziwa, Niwahakikishie ndugu zangu wa Rwanda na Tanzania kuwa nitawapa ushirikiano, nitasimamia utekelezaji wa makubaliano haya tuweze kufikia malengo tuliyoyakusudia”, alisema Ulega

Aidha, Waziri Ulega alimshukuru Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kufungua milango ya ushirikiano baina ya Tanzania na nchi nyingine akiongeza kuwa ushirikiano huo ni moja ya hatua zake za kuhakikisha Watanzania wanaendelea kunufaika kupitia rasilimali zao.

Kwa upande wake, Waziri wa Kilimo, Maliasili, na Mifugo wa Jamhuri ya Rwanda, Mhe. James Kabarebe alisema amefarijika na hatua hiyo iliyofikiwa kwani waliisubiri muda mrefu na ni imani yake kuwa tija kubwa itapatikana katika tasnia hiyo ya maziwa kupitia ushirikiano huo.